NAIBU WAZIRI OFISI YA RAISI MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA AFANYA ZIARA HANDENI.
Naibu Waziri Ofisi ya Raisi Menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora Mh. Dr. Marry Mwanjelwa amefanya ziara katika Wilaya ya Handeni Mkoani jana lengo likiwa ni kuongea na Watumishi wa umma na kutembelea walengwa na wanufaika wa TASAF.
Akizungumza katika kikao hicho na watumishi wa umma kilichofanyika katika ukumbi wa CCM Handeni Mh. Dr. Marry aliwataka watumishi wa umma kuwa wazalendo, kuzingatia uadilifu, uchapakazi, ubunifu na ushirikiano ambao una matokeo chanya.
Aliwaeleza watumishi hao kuwa serikali ya awamu ya tano ni ya kuchapa kazi kwa vitendo kwa kufuata kanuni taratibu na sheria na kwamba kila fedha iliyopangwa ifanye shughuli husika iliyopangiwa, watalaamu wahakikishe wanatoa ushauri wa kitaalamu wenye kuleta tija kwenye Halmashauri kupitia mabaza ya Madiwani.
Aidha, Mh. Dr. Marry aliwataka watumishi kuwahudumia wananchi kwa weledi na kwa wakati na wasichoke kwasababu wameajiriwa kwaajili ya kutumikia umma.
Pia amewataka watumishi kuvaa nguo za heshima na staha pamoja na lugha za staha wakati wanawahudumia wananchi na kwamba kila Halmashauri ihakikishe kamati za maadili zinafanya kazi ili kuimarisha weledi katika kazi.
Sambamba na hayo Mh. Dr. Marry aliwataka waajiri kuhakikisha wanasimamia maslahi ya wafanyakazi bila upendeleo na pale inapohitajika watumishi kueleweshwa waeleweshwe kwa wakati pia waajiri wawe wanafanya kikao na watumishi ili kusikiliza kero zao pamoja na kuwaelewesha masuala mbalimbali ya kiutumishi.
Baada ya kikao hicho Mh. Naibu waziri alitembelea wanufaika wa TASAF ambapo alifurahishwa jinsi ambavyo walengwa hao wanatumia fedha hizo kwa weledi na kuzalisha mpaka kufikia kuishi maisha bora, Pia aliwapongeza akina mama baada ya kutoa ushuhuda wa namna walivyozalisha fedha hizo kwa kuanzisha miradi mbalimbali ikiwepo ufugaji wa mifugo na kilimo hususani shamba la muhogo la ekari 15 alilotembelea katika kijiji cha Chanika Kofi.
Katibu Tawala Mkoa wa Tanga Mhandisi Zena Said aliwapongeza Viongozi wa Handeni kwa kuwa wachapa kazi lakini aliwahimiza viongozi kuwa na tabia ya kufanya vikao vya mara kwa mara na watumishi ili kutatua changamoto zao za kiutumishi na maslahi kwa kuwa changamoto zingine zinatatuliwa kwa kuwaelimisha lakini zile ambazo zitakuwa juu ya uwezo wao wazipeleke Wizara ya Utumishi kwani zitapatiwa ufumbuzi kwa wakati.
Mhandisi Zena aliwasihi pia watumishi kutoa mawazo chanya ambayo yanaweza kuleta maendeleo katika Tasisi bila woga na kwamba viongozi wawasikilize watumishi walioko chini yao bila kudharau mawazo yao mazuri yanayojenga “Ardhi ambayo ni tajiri kuliko yote ni makaburini kwasababu kule kumefukiwa watu wenye mawazo mazuri ambayo hawakuyasema sasa tufe tuzikwe tukiwa watupu kwa kuwa yale mawazo yetu mazuri tumeyatoa” alisema.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Handeni Mh. Athumani Malunda alimsihi Mh. Naibu Waziri kuongeza idadi ya watumishi wa Handeni hasa sekta ya Afya na Elimu kwani wamekuwa wachache sana kulingana na kazi zilizopo kiasi kwamba wanafanya kazi bila kupumzika.
Mh. Malunda alisema pamoja na uchache huo watumishi hao wanafanyakazi kwa ushirikiano ndiyo maana Handeni ikafanikiwa kuzalisha zao la muhogo kwa wingi chini ya uongozi mahiri wa Mkuu wa Wilaya ya Handeni Mh. Godwin Gondwe.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Handeni Mh.Godwin Gondwe aliwapongeza watumishi kwa kufanya kazi kwa weledi na ushirikiano mkubwa kwani wamekuwa wakionyesha ushirikiano pale ambapo palihitajika kufanyika jambo hasa katika kuhamasisha kilimo cha muhogo na kuwasihi kuendelea kuchapa kazi kwa weledi.
Wakati akizungumza na walengwa wa TASAF Mh. Gondwe aliwaeleza walengwa hao kuwa serikali inawapenda na kuwajali na pia imewaamini ndiyo maana ikawaletea fedha ili waweze kujikwamua kiuchumi kutoka katika hali duni kwenda katika maisha bora. Pia aliwapongeza kwa miradi wanayoibua ili kujiongezea kipato lakini aliwasihi walengwa hao kuendelea kuzalisha fedha hizo kwa kubuni miradi zaidi ambayo itawaongezea kipato kitakachotumika kukidhi mahitaji ya familia zao hususani kusomesha watoto na kujenga nyumba nzuri.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni Bw. William Makufwe akitoa taarifa kwa Naibu waziri wakati alipotembelea wanufaika wa TASAF katika Kata ya Ndolwa aliema katika Kata hiyo vijiji vilivyopata mradi wa TASAF ni vijiji 5 kati ya 8 ambapo kijiji cha Chanika Kofi alichotembelea kina walengwa 258 na toka mradi uanze wamepokea jumla ya kiasi cha shilingi milioni 236 kati ya hizo shilingi milioni 207 wanapewa walengwa na shilingi milioni 29 ni kwaajili ya ajira za muda. Aidha, Makufwe alisema kupitia hizo fedha za ajira za muda walengwa waliibua jumla ya miradi 78 na kati za hizo miradi 29 ilihusisha kilimo cha muhogo ambapo walilima jumla ya ekari 133 hivyo walengwa hao pia wamejikwamua kutoka kwenye uhaba wa chakula kwakuwa na uhakika wa chakula.
Mlengwa wa TASAF Bi. Elizabeth Dominick alisema wanamshukuru sana Mh. Raisi na wanamwombea kwa Mungu ambariki kwa kuwaletea fedha kwakuwa amewajengaea maisha mazuri maisha siyo kama zamani
MWISHO.
Naibu Waziri wa Utimishi Mh.Dr. Marry Mwanjelwa akizungumza na wanufaika wa TASAF katika kijiji cha Chanika Kofi
Katibu Tawala Mkoa wa Tanga Mhandisi Zena Said akizungumza na watumishi
Mwenyekiti CCM Wilaya Mh. Athumani Malunda akizungumza katika kikao cha watumishi
Mkuu wa Wilaya ya Handeni Mh. Godwin Gondwe akitoa nasaha kwa watumishi.
Mkurugenzi Mtendaji Bw. William Makufwe akitoa ripoti katika kijiji cha Chanika Kofi.
Watumishi wakifuatilia maagizo kutoka kwa viongozi.
Walengwa wakimsikiliza Naibu Waziri kwa furaha
Naibu Waziri Mh. Dr. Marry Mwanjelwa akicheza ngoma ya kizigua na wanufaika wa TASAF
Hakimiliki ©2017 Halmashauri ya Wilaya Handeni . Haki zote zimehifadhiwa